-->
logo
ads 720x90

Maelezo Mukhtasari Kuhusu Tarjama Ya Maana Ya Maneno Ya Qur-aan ‘Adhimu Somaqurani.com

Maelezo Mukhtasari Kuhusu Tarjama Ya Maana Ya Maneno Ya Qur-aan ‘Adhimu

Tarjama hii imeandaliwa kwa lengo la kuwawezesha wazungumzaji wa Kiswahili kufahamu maana sahihi ya Qur-aan Tukufu, nayo ni ya kwanza ya aina yake kwa kuwa inaendana na manhaj ya Nabiy wetu Muhammad (صلى لله عليه وآله سلم) na Salafus-Swaalih; Maswahaba (رضي الله عنهم), Taabi’iyn na waliowafuata kwa ihsaan mpaka Siku ya mwisho.

Kuna mambo mengi yanayoimaizi Tarjama hii kulinganisha na Tarjama zingine za Kiswahili. Kati ya mambo hayo ni:

  1. Imezithibitisha Sifa za Allaah (سبحانه وتعالى) zinazolaikiana na Utukufu Wake kama Alivyojithibitishia Yeye Mwenyewe na kuthibitishiwa pia na Rasuli Wake (صلى الله عليه آله وسلم) kama Sifa ya ‘Uluww (Kuweko juu), Istiwaa, Kusikia, Kuona, Mikono, Kuzungumza na Sifa nyinginezo zilizothibiti bila kuzifanyia ta'twiyl (kuzipinga, kukanusha uwezekano), wala tamthiyl (kumithilisha, kulinganisha), wala  takyiyf (kuainisha; namna gani), wala tahriyf (kupotosha na kubadilisha maana), kama vile inavyojulikana katika ‘Aqiydah ya Ahlus Sunnah wal Jamaa’ah..                         

  1. Imethibitisha masaail yote yahusianayo na mambo yaliyofichika (ghayb) kama Waumini kumwona Rabb wao Siku ya Qiyaamah na Peponi. Pia adhabu ya kaburi, Asw-Swiraatw (Njia ya kuvuka watu Siku ya Qiyaamah), Al-Miyzaan (Mizani) na mengineyo yaliyotajwa kwenye Qur-aan ‘Adhimu.   

  1. Tumechagua kwa uangalifu mkubwa misamiati inayowafikiana na makusudio ya Aayah.

  1. Tumefafanua baadhi ya vipengele vinavyohitajia kufafanuliwa kama masaail ya ki-‘Aqiydah na kadhalika. 

  1. Tumeweka sababu za kuteremshwa baadhi ya Aayah au Suwrah na mafunzo yanayopatikana.

  1. Tumetaja An-Naasikh (kinachofuta) na Al-Mansuwkh (kinachofutwa) pale tulipoweza.     
           
Kazi yoyote ya mwana Aadam bila shaka haikosi kasoro, nasi kwa Tawfiyq ya Allaah tumejitahidi kiasi cha uwezo wetu kuepuka hilo. Tunamwomba yeyote atakayegundua kosa, au kasoro, au mponyoko wowote ndani ya Tarjama hii, asisite kutujulisha haraka awezavyo, nasi tutashukuru kwa hilo. Atujulishe kupitia barua yetu pepe: info@somaqurani.com

Tunamwomba Allaah  (سبحانه وتعالى) kwa Fadhila Zake, Ukarimu Wake, Upaji Wake, na Ihsani Yake, Atutakabalie kazi hii,  hakika Yeye ni Mpaji Mno na Mkarimu Mno.